Katika kuadhimisha miaka 61 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo leo Aprili 26, 2025, imefanya shughuli mbalimbali ikiwemo usafi wa mazingira, upandaji wa miti, na ukaguzi wa miradi ya maendeleo.
Shughuli hizo zimefanyika katika maeneo ya Ofisi ya Halmashauri, Hospitali ya Wilaya ya Nsimbo, na Kata ya Itenka, zikiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Mpanda aliyewakilishwa na Afisa Tarafa. Watumishi wa Halmashauri, wananchi na viongozi mbalimbali wameshiriki kikamilifu katika shughuli hizo.
Katika kuhakikisha mazingira yanatunzwa, miti mbalimbali imepandwa katika maeneo tofauti ndani ya Kata ya Itenka ikiwa ni sehemu ya kampeni endelevu ya kutunza mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Aidha, viongozi wamefanya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa nyumba ya walimu katika Shule ya Sekondari Anna Lupembe iliyopo Kata ya Nsimbo, mradi unaokaribia kukamilika. Mradi huu ulianza tarehe 1 Oktoba 2024, na hadi sasa umetumia kiasi cha Shilingi 76,139,005.27 kati ya Shilingi 110,000,000 zilizotengwa, huku kiasi kilichobaki cha Shilingi 33,860,994.27 kikiendelea kusimamiwa ili kukamilisha kazi zilizobakia.
Walimu wa Shule ya Sekondari Anna Lupembe pamoja na viongozi wa Halmashauri wamemshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa fedha nyingi zilizowezesha ujenzi wa nyumba hiyo ya walimu.
Walimu hao wamesema kuwa mradi huu umekuwa suluhisho kubwa kwa changamoto ya kuishi mbali na shule, hali ambayo awali ilisababisha usumbufu mkubwa katika utekelezaji wa majukumu yao. Waliahidi kuhamia mara moja katika nyumba hiyo baada ya kukamilika, na kutimiza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa kwa manufaa ya wanafunzi na maendeleo ya sekta ya elimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Afisa Tarafa amewataka wananchi kuendelea kuenzi Muungano kwa vitendo kwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo, kulinda mazingira na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.
“Muungano Wetu ni Dhamana, Heshima na Tunu ya Taifa — Shiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025.”
Mpanda to Tabora road
Anuani ya Posta: P.O.Box 688 Mpanda
Simu : 025 295 5164
Simu: 025 295 5164
Barua pepe: ded@nsimbodc.go.tz
Hatimiliki@2016GWF.Haki zote zimehifadhiwa